Home » Tanzania » Balozi Seif Ali Idd amemhakikishia Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuwa hali ya Zanzibar ni shwari

Balozi Seif Ali Idd amemhakikishia Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuwa hali ya Zanzibar ni shwari

21 January 2016 | Tanzania

Makamu wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mheshimiwa Balozi Seif Ali Idd amemhakikishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kuwa hali ya Zanzibar ni shwari na Wazanzibari wanasubiri kutangaziwa tarehe ya kufanyika kwa uchaguzi.

Balozi Seif Ali Idd ameyasema hayo Ikulu jijini Dar es salaam leo tarehe 20 Januari, 2016 mara baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Rais Magufuli.

"Mimi nimekuja kumpa taarifa juu ya hali yetu Zanzibar inavyokwenda, nimemueleza kwamba Zanzibar ipo salama, Zanzibar ina utulivu na ina amani, nimeona nije nimueleze kwa kuwa yeye ni kiongozi wetu" alisisitiza Balozi Seif Ali Idd.

Makamu huyo wa pili wa Zanzibar ameongeza kuwa kutokana na uwepo wa amani na utulivu, wananchi wa Zanzibar wanaendelea na shughuli zao kama kawaida tofauti na inavyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.

"Hayo yanayoandikwa kwenye magazeti kuwa Zanzibar kuna fujo, Zanzibar kutatokea machafuko sio kweli, na kama unavyojua uchaguzi ulifutwa na tume ya uchaguzi na tunasubiri tarehe mpya ya uchaguzi itangazwe na tume ili tufanye uchaguzi" amebainisha Balozi Seif Ali Idd.

 

Gerson Msigwa.

Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU.

Dar es salaam.

20 Januari, 2016.

 

Ad