Home » Tanzania » KIWANDA CHA KUSAFISHA DHAHABU MWANZA CHAANZA UZALISHAJI RASMI

KIWANDA CHA KUSAFISHA DHAHABU MWANZA CHAANZA UZALISHAJI RASMI

22 April 2021 | Tanzania

Ni mageuzi makubwa kwenye Sekta ya Madini na uchumi kwa Taifa

Na. Steven Nyamiti, Mwanza.

Kiwanda  kikubwa  cha kusafisha Dhahabu Afrika Mashariki cha Mwanza Precious Metals Refinery (MPMR) ambacho ni Ubia kati ya Serikali kupitia Shirika la Madini la Taifa STAMICO kimeanza rasmi uzalishaji.

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO Dkt. Venance Mwasse wakati akishuhudia uzalishaji huo uliofanyika leo tarehe 21 Aprili, 2021 Jijini Mwanza kwa mara ya kwanza.

Dkt. Mwasse amesema kuwa, kiwanda hicho chenye uwezo wa kusafisha  Dhahabu kilo 480 kwa siku kimeanza na uzalishaji wa kilo  zaidi ya 40 za Dhahabu rasmi.

Aidha Dkt. Mwasse  amewaeleza wanahabari kutoka Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kuwa, kiwanda hicho kina uwezo wa kusafisha Dhahabu kwa asilimia 99.9 (purity) ya ubora  ambao ni wa kiwango cha juu cha Kimataifa.

"Chimbuko la kiwanda hiki ni matokeo ya mabadiliko ya Sheria ya Madini yaliyofanyika Mwaka 2017. STAMICO kwa kuunga mkono juhudi hizi za Serikali ikaingia ubia na wenzetu ambapo ndio tukaweka kiwanda hapa" amesema Dkt. Mwase.

Akifafanua sifa za kiwanda cha Mwanza Precious Metals Refinery amesema kuwa, mitambo yake inauwezo wa ziada wa kuongeza kiwango cha uzalishaji kwa kilo 960  za Dhahabu kwa siku.

Pia, kuanza kwa uzalishaji katika kiwanda hicho kutaiwezesha  Serikali kupata mapato kupitia tozo na mrabaha, kuongeza teknolojia za kisasa Nchini na kutoa ajira rasmi zaidi ya 100 na ajira nyingine zaidi ya 300 zisizo rasmi kwa watanzania.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongela ameipongeza Serikali kwa ujenzi wa kiwanda cha kisasa cha usafishaji Dhahabu jijini Mwanza. Mongela amesema yalifanyika mabadiliko ya Sheria ya ulinzi wa rasilimali zetu kwa kiwango kikubwa ujenzi wa kiwanda hicho ndio matokea ya Sheria hiyo.

"Kiwanda hicho na miundombinu husika itapelekea usafishaji wa madini ya Dhahabu kwa asilimia kubwa kufanyika hapa nchini.  STAMICO wametuhakikishia bei zitakazotumika hapa ni bei elekezi za soko la Kimataifa hivyo kupunguza utoroshaji wa madini kutafuta soko zaidi" amesema Mongela.

Mongela amesema uchumi wa  Mkoa wa Mwanza na Taifa utakua zaidi baada ya kutoa ajira nyingi, kodi kupatikana kwa njia salama zaidi na Dhahabu itakayopatikana kuweza kuhifadhiwa Benki kuu au kwingineko duniani.

Kuanza rasmi kwa usafishaji wa Dhahabu  katika kiwanda cha Mwanza Precious Metals Refinery  (MPMR) ni matokeo ya Serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Madini kuendelea Kuhamasisha  ujenzi wa viwanda vya kusafisha, kuchenjua na kuongeza thamani kufanyika hapa hapa nchini.

Katika kiwanda hicho, STAMICO ina ubia wa asilimia 25 na kampuni za Rozella General Trading LLC ya Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) pamoja na Kampuni ya ACME Consultant Engineers PTE Ltd ya Singapore zina ubia wa asilimia 75.

 

Ad