Home » Washirika » Rais Magufuli aweka jiwe la msingi ujenzi wa njia 8 barabara ya Kimara - Kibaha

Rais Magufuli aweka jiwe la msingi ujenzi wa njia 8 barabara ya Kimara - Kibaha

20 December 2018 | Washirika

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 19 Desemba, 2018 ameweka jiwe la msingi la upanuzi wa barabara ya Morogoro Jijini Dar es Salaam katika sehemu ya kuanzia Kimara hadi Kibaha yenye urefu wa Kilometa 19.2.

Upanuzi huo utahusisha kuongeza njia za magari kutoka 2 zilizopo sasa hadi 8, kujenga madaraja 6 na makalavati 36, na kujenga barabara ya juu (Flyover) katika eneo la Kibamba CCM kwenye makutano ya barabara inayotokea Bunju na barabara ya kwenda hospitali ya Mloganzila.

Sherehe za uwekaji jiwe la msingi la mradi huo zimefanyika katika eneo la Kimara Stopover na kuhudhuriwa na Mke wa Rais Mhe. Mama Janeth Magufuli, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Job Yustino Ndugai, Mawaziri, Wabunge, viongozi wa Dini, viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Paul Makonda.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mhandisi Patrick Mfugale amesema barabara ya Morogoro ni lango kuu la usafiri kati ya Jiji la Dar es Salaam lenye bandari kuu na mikoa mingi ya Tanzania Bara na nchi jirani, na kwamba upanuzi wake utasaidia kupunguza msongamano mkubwa wa magari takribani 50,000 yanayopita katika barabara hiyo kwa siku na utaokoa muda kutoka saa tatu zinazotumika kupita eneo hilo kwa sasa hadi nusu saa.

Amebainisha kuwa upanuzi wa barabara hiyo utafanyika kwa muda wa miezi 30 kuanzia tarehe 21 Julai 2018 na utagharimu shilingi Bilioni 141.56, fedha zote zinatolewa na Serikali ya Tanzania.

Akizungumza katika sherehe hizo Mhe. Rais Magufuli amewapongeza wananchi wa Dar es Salaam kwa kupatiwa mradi huo mkubwa na kubainisha kuwa pamoja na barabara hiyo Serikali ya Awamu ya Tano inaendelea kuboresha miundombinu ya Dar es Salaam ambapo barabara zenye jumla ya kilometa 212 zinajengwa kwa gharama ya shilingi Bilioni 660.

Kuhusu fidia kwa nyumba zilizovunjwa wakati wa upanuzi wa barabara hiyo Mhe. Rais Magufuli amewataka wanasiasa kuacha kuwapotosha wananchi kuwa watalipwa fidia, na amesema Serikali haitalipa fidia kwa mtu yeyote aliyejenga katika eneo la hifadhi ya barabara kwa mujibu wa sheria.

“Kuna wanasiasa wanataka waonekane wao ndio wanawatetea wananchi na wanasema Serikali itoe fidia, nataka niwaambie ndugu ukivamia barabara unatafuta umasikini, fidia haipo, fidia haipo, narudia fidia haipo” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli na kuwataka Watanzania kote nchini kuacha kuvamia maeneo ya hifadhi ya barabara na kujenga makazi.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kulipa kodi na kwamba Serikali itaendelea kuhakikisha kodi inayokusanywa inasimamiwa vizuri kwa kuelekezwa katika miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa barabara, kuendeleza elimu, afya na kuboresha upatikanaji wa maji ukiwemo mkoa wa Dar es Salaam ambao kwa sasa unapata maji kwa asilimia 75.

Mhe. Rais Magufuli amewaonya Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam waliokuwa wakichelewesha kuanza kwa ujenzi wa kituo kikuu cha mabasi kutokana na kubishana juu ya mkandarasi wa kukijenga na kubainisha kuwa “Nilikuwa nawafuatilia jinsi mnavyobishana na leo mngekuwa bado mnabishana nilipanga nitangaze kuondoa fedha hizo (shilingi Bilioni 50) na kupeleka mahali pengine, ndugu zangu viongozi naomba tutangulize maslahi ya wananchi, sio maslahi yetu binafsi”.

Mapema Spika wa Bunge Mhe. Job Yustino Ndugai amempongeza Mhe. Rais Magufuli kwa namna Serikali inavyosimamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo na kumhakikishia kuwa Bunge litaendelea kuunga mkono juhudi hizo zenye maslahi makubwa kwa Taifa.

Wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kazi kubwa inayofanywa na Serikali katika Mkoa huo ikiwemo kutatua tatizo la maji, kuimarisha miundombinu ya barabara na reli, kununua ndege na kuboresha uwanja wa ndege na kuboresha huduma za afya na elimu.

Wakati huo huo, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe amesema Serikali itaanza kutekeleza sheria ya kudhibiti uzito wa magari barabarani kuanzia Januari 2019 ili kuokoa uharibifu mkubwa wa barabara unaojitokeza katika barabara nyingi hivi sasa.

 

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Dar es Salaam

19 Desemba, 2018

Ad